Yesu Awatuma Wale Kumi Na Wawili
1 Yesu kisha akawaita wale kumi na wawili pamoja, akawapa mamlaka na uwezo wa kutoa pepo wachafu wote na kuponya magonjwa yote, 2 kisha akawatuma waende wakahubiri Ufalme wa Mungu na kuponya wagonjwa. 3 Akawaagiza akisema, "Msichukue chochote safarini: sio fimbo, wala mkoba, wala mkate, wala fedha, hata msichukue kanzu ya ziada. 4 Katika nyumba yoyote mwingiayo, kaeni humo hadi mtakapoondoka katika mji huo. 5 Kama watu wasipowakaribisha, mnapoondoka katika mji wao, kungʼuteni mavumbi kutoka kwenye miguu yenu ili kuwa ushuhuda dhidi yao." 6 Hivyo wale wanafunzi wakaondoka wakaenda kutoka kijiji hadi kijiji, wakihubiri habari njema na kuponya wagonjwa kila mahali.