1 Wakafika upande wa pili wa ziwa wakaingia katika nchi ya Wagerasi. 2 Yesu alipotoka kwenye mashua, mara mtu mmoja mwenye pepo mchafu akatoka makaburini akakutana naye. 3 Mtu huyu aliishi makaburini, wala hakuna aliyeweza kumzuia hata kwa kumfunga minyororo. 4 Kwa kuwa mara kwa mara alikuwa amefungwa minyororo mikononi na miguuni, lakini akaikata hiyo minyororo na kuzivunja zile pingu miguuni mwake. Hapakuwa na mtu yeyote aliyekuwa na nguvu za kumzuia. 5 Usiku na mchana alikuwa makaburini na milimani, akipiga kelele na kujikatakata kwa mawe.
6 Alipomwona Yesu kwa mbali, alimkimbilia, akapiga magoti mbele yake. 7 Akapiga kelele kwa nguvu akisema, "Una nini nami, Yesu, Mwana wa Mungu Aliye Juu Sana? Ninakusihi kwa jina la Mungu, usinitese!" 8 Kwa kuwa Yesu alikuwa amemwambia, "Mtoke mtu huyu, wewe pepo mchafu!"
9 Yesu akamuuliza, "Jina lako ni nani?"
Akamjibu, "Jina langu ni Legioni,5:9 Legioni maana yake ni Jeshi. kwa kuwa tuko wengi." 10 Akamsihi Yesu sana asiwapeleke nje ya nchi ile.
11 Palikuwa na kundi kubwa la nguruwe lililokuwa likilisha karibu kando ya kilima. 12 Wale pepo wachafu wakamsihi Yesu wakisema, "Tuamuru twende kwenye wale nguruwe. Turuhusu tuwaingie." 13 Basi Yesu akawaruhusu, nao wale pepo wachafu wakatoka, wakawaingia hao nguruwe. Lile kundi lilikuwa na nguruwe wapatao 2,000, nao wote wakateremkia gengeni kwa kasi, nao wakatumbukia ziwani na kuzama.
14 Wale watu waliokuwa wakichunga hao nguruwe wakakimbilia mjini na vijijini kueleza yaliyotukia. Watu wakatoka kwenda kuona hayo yaliyokuwa yametukia.