Pular para o conteúdo
Publicidade

Mateus 26

Shauri Baya La Kumuua Yesu

1 Yesu alipomaliza kusema hayo yote, akawaambia wanafunzi wake, 2 "Kama mnavyojua, baada ya siku mbili itakuwa Pasaka, naye Mwana wa Adamu atasalitiwa ili asulubiwe."

3 Basi viongozi wa makuhani na wazee wa watu wakakusanyika katika jumba la utawala la kuhani mkuu, jina lake Kayafa. 4 Wakafanya shauri ili kumkamata Yesu kwa siri na kumuua. 5 Lakini wakasema, "Isiwe wakati wa Sikukuu, kusitokee ghasia miongoni mwa watu."

Yesu Anapakwa Mafuta Huko Bethania

6 Yesu alikuwa Bethania nyumbani mwa Simoni aliyekuwa na ukoma, 7 naye mwanamke mmoja akamjia akiwa na chupa ya marhamu yenye manukato ya thamani kubwa; akayamimina kichwani mwa Yesu alipokuwa ameketi mezani kula chakula.

8 Lakini wanafunzi wake walipoona hayo wakakasirika, wakasema, "Upotevu huu wote ni wa nini? 9 Manukato haya yangeuzwa kwa bei kubwa, na fedha hizo wakapewa maskini."

10 Yesu, akijua jambo hili, akawaambia, "Mbona mnamsumbua huyu mwanamke? Yeye amenitendea jambo zuri sana. 11 Maskini mtakuwa nao siku zote, lakini mimi hamtakuwa nami siku zote. 12 Alipomiminia haya manukato kwenye mwili wangu, amefanya hivyo ili kuniandaa kwa ajili ya maziko yangu. 13 Amin, nawaambia, mahali popote ulimwenguni ambapo hii Injili itahubiriwa, jambo hili alilolitenda huyu mwanamke litatajwa pia kwa ukumbusho wake."

Yuda Akubali Kumsaliti Yesu

14 Kisha mmojawapo wa wale kumi na wawili, aitwaye Yuda Iskariote, alikwenda kwa viongozi wa makuhani 15 na kuuliza, "Mtanipa nini nikimtia Yesu mikononi mwenu?" Wakamlipa vipande thelathini vya fedha. 16 Tangu wakati huo Yuda akawa anatafuta wakati uliofaa wa kumsaliti Yesu.

Yesu Ala Pasaka Pamoja Na Wanafunzi

17 Siku ya kwanza ya Sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu, wanafunzi walimjia Yesu wakamuuliza, "Unataka twende wapi ili tukuandalie mahali pa kula Pasaka?"

18 Akajibu, "Nendeni kwa mtu fulani huko mjini, mkamwambie, Mwalimu asema hivi: Saa yangu imekaribia. Nitaiadhimisha Pasaka pamoja na wanafunzi wangu katika nyumba yako.’ " 19 Hivyo wanafunzi wakafanya kama vile Yesu alivyokuwa amewaelekeza, nao wakaandaa Pasaka.

20 Ilipofika jioni, Yesu alikuwa ameketi mezani pamoja na wale wanafunzi wake kumi na wawili. 21 Nao walipokuwa wakila, Yesu akasema, "Amin, nawaambia, mmoja wenu atanisaliti."

22 Wakahuzunika sana, wakaanza kumuuliza mmoja baada ya mwingine, "Je, ni mimi Bwana?"

23 Yesu akawaambia, "Yule aliyechovya mkono wake katika bakuli pamoja nami ndiye atakayenisaliti. 24 Mwana wa Adamu anaenda zake kama vile alivyoandikiwa. Lakini ole wake mtu yule amsalitiye Mwana wa Adamu. Ingekuwa heri kwake mtu huyo kama hangezaliwa!"

25 Kisha Yuda, yule mwenye kumsaliti, akasema, "Je, ni mimi Rabi?"

Yesu akajibu, "Naam, wewe mwenyewe umesema."

Kuanzishwa Kwa Meza Ya Bwana

26 Walipokuwa wanakula, Yesu akachukua mkate, akashukuru, akaumega, na kuwapa wanafunzi wake, akisema, "Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu."

27 Kisha akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, akisema, "Nyweni nyote katika kikombe hiki. 28 Hii ndiyo damu yangu ya Agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi.

Veja também