Pular para o conteúdo
Publicidade

Mateus 4

Kujaribiwa Kwa Yesu

1 Kisha Yesu akaongozwa na Roho Mtakatifu kwenda nyikani ili akajaribiwe na ibilisi. 2 Baada ya kufunga siku arobaini usiku na mchana, hatimaye akaona njaa. 3 Mjaribu akamjia na kumwambia, "Ikiwa wewe ndiye Mwana wa Mungu, amuru mawe haya yawe mikate."

4 Lakini Yesu akajibu, "Imeandikwa: Mtu haishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.’ "

5 Ndipo ibilisi akamchukua Yesu mpaka mji mtakatifu na kumweka juu ya mnara mrefu wa Hekalu, 6 akamwambia, "Kama wewe ndiwe Mwana wa Mungu jitupe chini. Kwa kuwa imeandikwa:

" Atakuagizia malaika zake,

nao watakuchukua mikononi mwao

ili usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe.’ "

7 Yesu akamjibu, "Pia imeandikwa: Usimjaribu Bwana Mungu wako.’ "

8 Kwa mara nyingine, ibilisi akamchukua Yesu mpaka kwenye kilele cha mlima mrefu na kumwonyesha falme zote za dunia na fahari zake, 9 kisha akamwambia, "Nitakupa hivi vyote kama ukinisujudia na kuniabudu."

10 Yesu akamwambia, "Ondoka mbele yangu, Shetani! Kwa maana imeandikwa, Mwabudu Bwana Mungu wako, na umtumikie yeye peke yake.’ "

11 Ndipo ibilisi akamwacha, nao malaika wakaja na kumhudumia.

Veja também