Publicidade

Mateus 26

Mpango wa kumwua Yesu

1 Ikawa Yesu alipomaliza maneno hayo yote, aliwaambia wanafunzi wake, 2 Mnajua ya kuwa baada ya siku mbili itakuwa Pasaka, na Mwana wa Adamu atasalitiwa asulubiwe.3 Wakati ule wakuu wa makuhani, na wazee wa watu, wakakusanyika katika behewa ya Kuhani Mkuu, jina lake Kayafa; 4 wakafanya shauri pamoja, ili wamkamate Yesu kwa hila na kumwua. 5 Lakini wakasema, Isiwe wakati wa sikukuu, isije ikatokea ghasia miongoni mwa watu.

Yesu apakwa mafuta Bethania

6 Naye Yesu alipokuwapo Bethania katika nyumba ya Simoni mwenye ukoma, 7 mwanamke mwenye kibweta cha marhamu ya thamani kubwa alimkaribia akaimimina kichwani pake alipoketi chakulani. 8 Wanafunzi wake walipoona, wakakasirika, wakasema, Ni wa nini upotevu huu? 9 Maana marhamu hii ingaliweza kuuzwa kwa fedha nyingi wakapewa maskini. 10 Yesu akatambua akawaambia, Mbona mnamtaabisha mwanamke? Maana ni kazi njema aliyonitendea mimi. 11 Kwa maana siku zote mnao maskini pamoja nanyi; lakini mimi hamko nami siku zote. 12 Maana kwa kunimwagia mwili wangu marhamu hiyo, ametenda hivyo ili kuniweka tayari kwa maziko yangu. 13 Amin, nawaambieni, Kila patakapohubiriwa Injili hii katika ulimwengu wote, tendo hilo alilolitenda huyu litatajwa pia kwa kumbukumbu yake.

Yuda akubali kumsaliti Yesu

14 Wakati huo mmoja wa wale Kumi na Wawili, jina lake Yuda Iskarioti, aliwaendea wakuu wa makuhani, 15 akasema, Ni nini mtakachonipa, nami nitamsaliti kwenu? Wakampimia vipande thelathini vya fedha.16 Tokea wakati huo akawa akitafuta nafasi apate kumsaliti.

Yesu katika Pasaka pamoja na wanafunzi

17 Katika siku ya kwanza ya mikate isiyotiwa chachu, wanafunzi wake wakamwendea Yesu, wakamwambia, Ni wapi utakapo tukuandalie uile Pasaka?18 Akasema, Nendeni mjini kwa mtu fulani, mkamwambie, Mwalimu asema, Majira yangu ni karibu; kwako nitafanya Pasaka pamoja na wanafunzi wangu. 19 Wanafunzi wakafanya kama Yesu alivyowaagiza, wakaiandaa Pasaka. 20 Basi kulipokuwa jioni aliketi chakulani pamoja na wale Kumi na Wawili. 21 Nao walipokuwa wakila, alisema, Amin, nawaambia, Mmoja wenu atanisaliti. 22 Wakahuzunika sana, wakaanza kumwuliza mmoja mmoja, Ni mimi, Bwana? 23 Akajibu akasema, Yeye aliyetia mkono wake pamoja nami katika bakuli, ndiye atakayenisaliti. 24 Mwana wa Adamu aenda zake, kama alivyoandikiwa; lakini ole wake mtu yule ambaye amsaliti Mwana wa Adamu! Ingekuwa heri kwake mtu yule kama asingalizaliwa. 25 Yuda, yule mwenye kumsaliti, akajibu, akasema, Ni mimi, Rabi? Akamwambia, Wewe umesema.

Kuanzishwa kwa chakula cha Bwana

26 Nao walipokuwa wakila Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake, akasema, Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu 27 Akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, akisema, Kuyweni nyote katika hiki; 28 kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi.

Veja também

Publicidade
Bíblia Online Bíblia Online

Bíblia Online • Versão: 2026-06-28_14-13-17-