Publicidade

Jeremias 47

Ujumbe Kuhusu Wafilisti

1 Hili ndilo neno la Bwana lililomjia nabii Yeremia kuhusu Wafilisti, kabla Farao hajaishambulia Gaza:

2 Hili ndilo asemalo Bwana:

"Tazama jinsi maji yanavyoinuka huko kaskazini,

yatakuwa mafuriko yenye nguvu sana.

Yataifurikia nchi na vitu vyote vilivyomo ndani yake,

miji na wale waishio ndani yake.

Watu watapiga kelele;

wote waishio katika nchi wataomboleza

3 kwa sauti ya kwato za farasi waendao mbio,

kwa sauti ya magari ya adui

na mngurumo wa magurudumu yake.

Baba hawatageuka kuwasaidia watoto wao,

mikono yao italegea.

4 Kwa maana siku imewadia

kuwaangamiza Wafilisti wote

na kuwakatilia mbali walionusurika wote

ambao wangeweza kusaidia Tiro na Sidoni.

Bwana anakaribia kuwaangamiza Wafilisti,

mabaki toka pwani za Kaftori.

5 Gaza atanyoa kichwa chake katika kuomboleza,

Ashkeloni atanyamazishwa.

Enyi mabaki kwenye tambarare,

mtajikatakata wenyewe mpaka lini?

6 "Mnalia, ‘Aa, upanga wa Bwana,

utaendelea mpaka lini ndipo upumzike?

Rudi ndani ya ala yako;

acha na utulie.’

7 Lakini upanga utatuliaje

wakati Bwana ameuamuru,

wakati ameuagiza kuishambulia Ashkeloni

pamoja na pwani yake?"

Veja também

Publicidade
Bíblia Online Bíblia Online

Bíblia Online • Versão: 2026-06-16_06-50-08-