4 Mnapokuja kwake, yeye aliye Jiwe lililo hai, lililokataliwa na wanadamu bali kwa Mungu ni teule na la thamani kwake, 5 ninyi nanyi, kama mawe yaliyo hai, mnajengwa kuwa nyumba ya kiroho, ili mpate kuwa ukuhani mtakatifu, mkitoa dhabihu za kiroho zinazokubaliwa na Mungu kupitia kwa Isa Al-Masihi. 6 Kwa maana imeandikwa katika Maandiko:
"Tazama, naweka katika Sayuni,
jiwe la pembeni teule lenye thamani,
na yeyote atakayemwamini
hataaibishwa kamwe."
7 Kwenu ninyi mnaoamini, jiwe hili ni la thamani. Lakini kwao wasioamini,
"Jiwe walilolikataa waashi
limekuwa jiwe kuu la pembeni,"
8 tena,
"Jiwe lenye kuwafanya watu wajikwae,
na mwamba wa kuwaangusha."
Wanajikwaa kwa sababu hawakulitii lile neno, kama walivyowekewa tangu zamani.