Mafuta ya mjane
1 Mke wa mmoja wa wana wa manabii akamlilia Al-Yasa, akamwambia, "Mtumishi wako, mume wangu, amekufa, nawe unajua alikuwa anamcha Mwenyezi Mungu. Lakini sasa yule anayemdai anakuja kuchukua wanangu wawili kama watumwa wake."
2 Al-Yasa akamjibu, "Nitawezaje kukusaidia? Niambie, una nini ndani ya nyumba yako?"
Akasema, "Mtumishi wako hana kitu chochote kabisa, isipokuwa mafuta kidogo."
3 Al-Yasa akasema, "Zunguka kwa majirani zako wote ukaombe vyombo vitupu. Usiombe vichache. 4 Kisha ingia ndani na ujifungie mlango, wewe na wanao. Mimina mafuta kwenye vyombo vyote, na kila kimoja kinapojaa, kiweke kando."
5 Yule mjane akaondoka na kujifungia ndani, yeye na wanawe. Wao wakamletea vyombo, naye akaendelea kumimina mafuta. 6 Vyombo vyote vilipojaa, akamwambia mwanawe, "Niletee chombo kingine."
Lakini mwanawe akajibu, "Hakuna chombo kingine kilichobaki." Basi mafuta yakakoma kutiririka.
7 Yule mwanamke akaenda akamwambia yule mtu wa Mungu, naye mtu wa Mungu akasema, "Nenda ukayauze hayo mafuta ulipe madeni yako. Wewe na wanao mnaweza kuishi kwa kile kinachosalia."