1 BWANA, Mungu wako, atakapokutia katika nchi uendayo kuimiliki, atakapoyang'oa mataifa mengi watoke mbele yako, Mhiti, na Mgirgashi, na Mwamori, na Mkanaani, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi, mataifa saba makubwa yenye nguvu kukupita wewe; 2 wakati BWANA, Mungu wako, atakapowatoa mbele yako, nawe utawapiga; wakati huo ndipo uwaondoe kabisa; usifanye agano nao, wala kuwahurumia; wala usioane nao; 3 binti yako usimwoze kwao wala mtoto wako wa kiume kuoa kwao. 4 Kwa kuwa atamkengeusha mwanao asinifuate, ili wapate kuabudu miungu mingine; ndipo itakapowaka hasira ya BWANA juu yenu, naye atakuangamiza upesi. 5 Lakini watendeni hivi; zivunjeni madhabahu zao zibomoeni nguzo zao, yakateni maashera yao, ziteketezeni kwa moto sanamu zao za kuchonga.
6 Kwa maana wewe u taifa takatifu kwa BWANA, Mungu wako; BWANA Mungu wako, amekuchagua kuwa watu wake hasa, zaidi ya mataifa yote walioko juu ya uso wa nchi. 7 BWANA hakuwapenda ninyi, wala hakuwachagua ninyi, kwa sababu mlikuwa wengi kuliko mataifa yote, maana mlikuwa wachache kuliko watu wote; 8 bali kwa sababu BWANA anawapenda, na kwa sababu alitaka kukitimiza kiapo chake alichowaapia baba zenu, ndiyo sababu BWANA akawatoa kwa mkono wa nguvu, akawakomboa katika nyumba ya utumwa, katika mkono wa Farao, mfalme wa Misri. 9 Basi jueni ya kuwa BWANA, Mungu wenu, ndiye Mungu; Mungu mwaminifu, ashikaye agano lake na rehema zake kwao wampendao, na kushika amri zake, hadi vizazi elfu; 10 naye huwalipa wamchukiao mbele ya uso wao, kuwaangamiza. Hatakuwa mlegevu kwake yeye amchukiaye, atamlipa mbele ya uso wake. 11 Basi zishike amri, na sheria, na hukumu ninazokuamuru leo, uzitende.
12 Na itakuwa, kwa sababu mnazisikiliza hukumu hizi, na kuzishika na kuzitenda, basi BWANA, Mungu wako, atakutimilizia agano na rehema aliyowaapia baba zako; 13 naye atakupenda na kukubariki na kukuongeza tena ataubariki uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, nafaka zako na divai yako, na mafuta yako, kuongezeka kwa ng'ombe na kondoo wako, katika nchi aliyowaapia baba zako kuwa atakupa. 14 Utabarikiwa kuliko mataifa yote; hakutakuwa na mwanamume wala mwanamke aliye tasa kati yenu; wala kati ya wanyama wenu wa kufugwa. 15 Na BWANA atakuondolea ugonjwa wote; wala hatatia juu yako maradhi yoyote mabaya uyajuayo ya Misri, lakini atayaweka juu ya wote wakuchukiao. 16 Nawe angamiza mataifa yote atakayokupa BWANA, Mungu wako; jicho lako lisiwahurumie, wala usiitumikie miungu yao; kwani jambo hilo litakuwa ni mtego kwako. 17 Nawe kama ukisema moyoni mwako, Mataifa haya ni mengi kuliko mimi; nitawatoaje katika milki yao? 18 Usiwaogope; kumbuka sana BWANA, Mungu wako, alivyomfanya Farao na Misri yote; 19 uyakumbuke hayo majaribu makuu yaliyoyaona macho yako, na hizo ishara, na maajabu, na mkono wa nguvu, na mkono ulionyoka, aliokutolea nje BWANA, Mungu wako; ndivyo atakavyowafanya BWANA, Mungu wako, mataifa yote unaowaogopa. 20 Tena BWANA, Mungu wako, atampeleka mavu kati yao, hata hao watakaosalia, hao wajifichao, waangamie mbele zako. 21 Usiingiwe na hofu kwa sababu yao; kwa kuwa BWANA, Mungu wako, yuko pamoja nawe, Mungu mkuu, mwenye utisho. 22 Naye BWANA, Mungu wako, atayatupilia mbali mataifa yale mbele yako kidogo kidogo; haikupasi kuwaangamiza kwa mara moja, wasije wakaongezeka kwako wanyama wa mwitu. 23 Ila BWANA, Mungu wako, atawatoa mbele yako, atawatia mashaka, mashaka makuu, hata waishe kuangamizwa. 24 Na wafalme wao atakutilia mkononi mwako, nawe utalipoteza jina lao litoke chini ya mbingu; hapana mtu atakayeweza kusimama mbele yako, hata utakapokwisha kuwaangamiza. 25 Sanamu za kuchonga za miungu yao mtaziteketeza kwa moto; usitamani fedha wala dhahabu iliyo juu yao, wala usiitwae iwe yako usije ukanaswa nayo; kwa maana ni machukizo kwa BWANA, Mungu wako; 26 na usitie kitu kilicho haramu ndani ya nyumba yako, usije ukalaaniwa kama haramu hiyo; ukichukie kabisa na kukikataa kabisa, kwa kuwa ni kitu kilicholaaniwa.