1 Ndipo Yona akamwomba BWANA, Mungu wake, akiwa katika tumbo la yule samaki, 2 Akasema,
Nilimlilia BWANA kwa sababu ya shida yangu,
Naye akaniitikia;
Katika tumbo la kuzimu niliomba,
Nawe ukasikia sauti yangu.
3 Maana ulinitupa vilindini,
Ndani ya moyo wa bahari;
Gharika ya maji ikanizunguka pande zote;
Mawimbi yako yote na gharika zako zote zimepita juu yangu.
4 Nami nikasema, Nimetupwa mbali na macho yako;
Lakini nitatazama tena kukabili hekalu lako takatifu.
5 Maji yalinizunguka, hata nafsini mwangu;
Vilindi vilinizunguka;
Mwani ulikizinga kichwa changu;
6 Nilishuka hata pande za chini za milima;
Hiyo nchi ambayo mapingo yake yanafunga hata milele;
Lakini umeipandisha nafsi yangu kutoka humo shimoni,
Ee BWANA, Mungu wangu,
7 Roho yangu ilipozimia ndani yangu,
Nilimkumbuka BWANA;
Maombi yangu yakakufikia,
Katika hekalu lako takatifu.
8 Watu waangaliao mambo ya ubatili na uongo
Hujitenga na rehema zao wenyewe.
9 Lakini mimi nitakutolea sadaka kwa sauti ya shukrani;
Nitaziondoa nadhiri zangu.
Wokovu hutoka kwa BWANA.
10 BWANA akasema na yule samaki, naye akamtapika Yona katika pwani.