Publicidade

Isaías 35

Furaha ya waliokombolewa

1 Jangwa na nchi kame vitafurahi;

nyika itashangilia na kuchanua maua.

Kama waridi, 2 litachanua maua,

litashangilia sana na kupaza sauti kwa furaha.

Litapewa utukufu wa Lebanoni,

fahari ya Karmeli na Sharoni;

wataona utukufu wa Mwenyezi Mungu,

fahari ya Mungu wetu.

3 Itieni nguvu mikono iliyo dhaifu,

yafanyeni imara magoti yaliyolegea,

4 waambieni wale wenye mioyo ya hofu,

"Kuweni hodari, msiogope;

tazama, Mungu wenu atakuja kulipa kisasi,

pamoja na ujira wake,

atakuja na kuwaokoa."

5 Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa

na masikio ya viziwi yatazibuliwa.

6 Ndipo kilema atarukaruka kama kulungu,

nao ulimi wa aliye bubu utapaza sauti kwa shangwe.

Maji yatatiririka kwa kasi katika nyika,

na vijito katika jangwa.

7 Mchanga wa moto utakuwa bwawa la maji,

ardhi yenye kiu itabubujika chemchemi.

Maskani ya mbweha walikolala hapo awali

patamea nyasi, matete na mafunjo.

8 Nako kutakuwa na njia kuu,

nayo itaitwa Njia ya Utakatifu.

Wasio safi hawatapita juu yake;

itakuwa ya wale wanaotembea katika Njia Ile;

yeye asafiriye juu yake,

ajapokuwa mjinga, hatapotea.

9 Huko hakutakuwa na simba,

wala mnyama mkali hatapita njia hiyo;

hawatapatikana humo.

Ila waliokombolewa tu ndio watakaopita huko,

10 waliokombolewa na Mwenyezi Mungu watarudi.

Wataingia Sayuni wakiimba;

furaha ya milele itakuwa juu ya vichwa vyao.

Watapata furaha na shangwe;

huzuni na majonzi vitakimbia.

Veja também

Publicidade
Bíblia Online Bíblia Online

Bíblia Online • Versão: 2026-06-15_21-32-39-