Publicidade

Provérbios 12

1 Kila apendaye mafundisho hupenda maarifa;

Bali yeye achukiaye kulaumiwa ni kama mnyama.

2 Mtu mwema atapata upendeleo kwa BWANA;

Bali mtu wa hila atahukumiwa naye.

3 Mtu hatathibitika kwa njia ya uovu;

Shina la mwenye haki halitaondolewa kamwe.

4 Mwanamke mwema ni taji la mumewe;

Bali aaibishaye ni kama kuoza mifupani mwake.

5 Mawazo ya mwenye haki ni adili;

Bali mashauri ya mtu mwovu ni hadaa.

6 Maneno ya waovu huotea damu;

Bali kinywa cha wanyofu kitawaokoa.

7 Waovu huangamia, hata hawako tena;

Bali nyumba ya mwenye haki itasimama.

8 Mtu atasifiwa kwa kadiri ya akili zake;

Bali mwenye moyo wa ukaidi atadharauliwa.

9 Afadhali mtu anayedharauliwa, ikiwa ana mtumwa,

Kuliko ajisifuye, ikiwa anahitaji chakula.

10 Mwenye haki huufikiri uhai wa mnyama wake;

Bali huruma za mtu mwovu ni ukatili.

11 Alimaye shamba lake atakuwa na chakula tele;

Bali afuataye mambo ya upuzi hana ufahamu.

12 Asiye haki hutamani nyavu za wabaya;

Bali shina lao wenye haki huleta matunda.

13 Katika kosa la midomo kuna mtego kwa mbaya;

Bali mwenye haki atatoka katika taabu.

14 Mtu atashiba mema kwa matunda ya kinywa chake;

Na atarudishiwa matendo ya mikono yake.

15 Njia ya mpumbavu imenyoka machoni pake mwenyewe;

Bali yeye aliye na hekima husikiliza shauri.

16 Ghadhabu ya mpumbavu hujulikana mara;

Bali mtu mwerevu husitiri aibu.

17 Atamkaye maneno ya kweli hufunua haki;

Bali shahidi wa uongo hutamka hila.

18 Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga;

Bali ulimi wa mwenye haki ni afya.

19 Mdomo wa kweli utathibitishwa milele;

Bali ulimi wa uongo ni wa kitambo tu.

20 Hila imo mioyoni mwao wafikirio uovu;

Bali wafanyao mashauri ya amani, kwao kuna furaha.

21 Mwenye haki hatapatikana na msiba wowote;

Bali wasio haki watajazwa mabaya.

22 Midomo ya uongo ni chukizo kwa BWANA;

Bali watendao uaminifu ndio furaha yake.

23 Mwanadamu mwenye busara husitiri maarifa;

Bali moyo wa wapumbavu hutangaza upumbavu.

24 Mkono wa mwenye bidii utatawala;

Bali mvivu atalipishwa kodi.

25 Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha;

Bali neno jema huufurahisha.

26 Mwenye haki ni kiongozi wa mwenzake;

Bali njia ya wasio haki huwakosesha.

27 Mtu mvivu hapiki mawindo yake;

Bali mwenye bidii anazo mali za thamani.

28 Katika njia ya haki kuna uhai;

Wala hakuna mauti katika mapito yake.

Veja também

Publicidade
Bíblia Online Bíblia Online

Bíblia Online • Versão: 2026-06-16_18-40-07-