1 Jawabu la upole hugeuza hasira;
Bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.
2 Ulimi wa mwenye hekima hutamka maarifa vizuri;
Bali vinywa vya wapumbavu humwaga upumbavu.
3 Macho ya BWANA yako kila mahali;
Yakimchunguza mbaya na mwema.
4 Ulimi safi ni mti wa uzima;
Bali ukorofi wa ulimi huvunja moyo.
5 Mpumbavu hudharau kurudiwa na babaye;
Bali yeye aangaliaye maonyo hupata busara.
6 Katika nyumba ya mwenye haki mna akiba nyingi;
Bali mapato ya mtu mbaya huwa taabu tu.
7 Midomo ya mwenye haki hueneza maarifa;
Bali moyo wa mpumbavu haufanyi hivyo.
8 Sadaka ya mtu mbaya ni chukizo kwa BWANA;
Bali maombi ya mtu mnyofu ni furaha yake.
9 Njia ya mtu mbaya ni chukizo kwa BWANA;
Bali humpenda mtu afuatiaye wema.
10 Adhabu kali ina yeye aiachaye njia;
Naye achukiaye kukemewa atakufa.
11 Kuzimu na Uharibifu viko wazi mbele za BWANA;
Si zaidi basi, mioyo ya wanadamu?
12 Mwenye mzaha hapendi kukaripiwa;
Wala yeye hawaendei wenye hekima.
13 Moyo wa furaha huchangamsha uso;
Bali kwa huzuni ya moyo roho hupondeka.
14 Moyo wa mwenye ufahamu hutafuta maarifa;
Bali kinywa cha wapumbavu hula upumbavu.
15 Siku zote za mtu ateswaye ni mbaya;
Bali ukunjufu wa moyo ni karamu ya daima.
16 Kuwa na mali chache pamoja na kumcha BWANA;
Ni bora kuliko mali nyingi pamoja na taabu.
17 Chakula cha mboga palipo na upendo;
Ni bora kuliko ng'ombe aliyenona pamoja na kuchukiana.
18 Mtu wa hasira huchochea ugomvi;
Bali asiye mwepesi wa hasira hutuliza mashindano.
19 Njia ya mtu mvivu ni kama boma la miiba;
Bali mapito yao wenye unyofu hufanyika njia kuu.
20 Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye;
Bali mpumbavu humdharau mamaye.
21 Upumbavu ni furaha kwake aliyepungukiwa na akili;
Bali mwenye ufahamu huunyosha mwenendo wake.
22 Pasipo ushauri mipango vuhunjika;
Bali kwa wingi wa washauri huthibitika.
23 Mtu hulifurahia jibu la kinywa chake;
Na neno linenwalo wakati wa kufaa ni jema kama nini!
24 Kwa mtu mwenye akili njia ya uhai huenda juu;
Ili atoke katika kuzimu chini.
25 BWANA ataing'oa nyumba ya mwenye kiburi;
Bali atauthibitisha mpaka wa mjane.
26 Ushauri mbaya ni chukizo kwa BWANA;
Bali maneno yapendezayo ni safi.
27 Atamaniye faida huifadhaisha nyumba yake mwenyewe;
Bali achukiaye zawadi ataishi.
28 Moyo wa mwenye haki hufikiri jinsi atakavyojibu;
Bali kinywa cha wasio haki humwaga mabaya.
29 BWANA yuko mbali na wasio haki;
Bali huisikia sala ya mwenye haki.
30 Mng'ao wa macho huufurahisha moyo;
Habari njema huinenepesha mifupa.
31 Sikio lisikilizalo lawama yenye uhai
Litakaa kati yao wenye hekima.
32 Akataaye maonyo huidharau nafsi yake mwenyewe;
Bali yeye asikilizaye lawama hujipatia ufahamu.
33 Kumcha BWANA ni maonyo ya hekima;
Na kabla ya heshima hutangulia unyenyekevu.