Publicidade

Provérbios 10

KITABU CHA PILI

Mithali za Sulemani

1 Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye;

Bali mwana mpumbavu ni mzigo wa mamaye.

2 Hazina za uovu hazifaidii kitu;

Bali haki huokoa na mauti.

3 BWANA hataiacha nafsi ya mwenye haki ife na njaa;

Bali tamaa ya mtu mwovu huisukumia mbali.

4 Atendaye mambo kwa mkono mlegevu huwa maskini;

Bali mkono wake aliye na bidii hutajirisha.

5 Akusanyaye wakati wa joto ni mwana mwenye hekima;

Bali asinziaye wakati wa mavuno ni mwana mwenye kuaibisha.

6 Baraka humkalia mwenye haki kichwani;

Bali jeuri hufunika kinywa chake mtu mwovu.

7 Kuwakumbuka wenye haki huwa na baraka;

Bali jina la mtu mwovu litaoza.

8 Aliye na akili moyoni mwake atapokea agizo;

Bali mpumbavu mwenye maneno mengi ataanguka.

9 Aendaye kwa unyofu huenda salama;

Bali apotoshaye njia zake atajulikana.

10 Akonyezaye kwa jicho huleta masikitiko;

Bali mpumbavu mwenye maneno mengi ataanguka.

11 Kinywa chake mwenye haki ni chemchemi ya uzima;

Bali jeuri hufunika kinywa chake mtu mwovu,

12 Kuchukiana huleta fitina;

Bali kupendana husitiri makosa yote.

13 Hekima hupatikana midomoni mwa mwenye ufahamu;

Bali fimbo hufaa kwa mgongo wake asiye na ufahamu.

14 Watu wenye akili huweka akiba ya maarifa;

Bali kinywa cha mpumbavu ni uangamivu ulio karibu.

15 Mali ya tajiri ndio ngome yake;

Ufukara wa maskini ndio umwangamizao.

16 Kazi yake mwenye haki huuelekea uzima;

Mazao ya wabaya huielekea dhambi.

17 Akubaliye kurudiwa huwa katika njia ya uzima;

Bali yeye aachaye maonyo hukosa.

18 Yeye afichaye chuki ana midomo ya uongo,

Na yeye asingiziaye ni mpumbavu.

19 Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na maovu;

Bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili.

20 Ulimi wa mwenye haki ni kama fedha safi;

Moyo wa mtu mbaya haufai kitu.

21 Midomo ya mwenye haki hulisha watu wengi;

Bali wapumbavu hufa kwa kuwa hawana ufahamu.

22 Baraka ya BWANA hutajirisha,

Wala hachanganyi huzuni nayo.

23 Kwa mpumbavu kutenda maovu ni kama mchezo;

Bali mtu mwenye ufahamu ana hekima.

24 Aogopacho mtu asiye haki ndicho kitakachomjilia;

Na wenye haki watapewa matakwa yao.

25 Kisulisuli kikiisha pita asiye haki hayuko tena;

Bali mwenye haki ni msingi wa milele.

26 Kama siki menoni, na kama moshi machoni,

Ndivyo alivyo mtu mvivu kwa hao waliomwajiri.

27 Kumcha BWANA kwaongeza siku za mtu;

Bali miaka yao wasio haki itapunguzwa.

28 Matumaini yao wenye haki yatakuwa furaha;

Bali matarajio yao wasio haki yatapotea.

29 Njia ya BWANA ni kimbilio lake mtu mkamilifu;

Bali ni uharibifu kwao watendao maovu.

30 Mwenye haki hataondolewa milele;

Bali wasio haki hawatakaa katika nchi.

31 Kinywa cha mwenye haki hutoa hekima;

Bali ulimi wa ukaidi utakatiliwa mbali.

32 Midomo ya mwenye haki huyajua yatakayokubaliwa;

Bali kinywa chao wasio haki hunena ukaidi.

Veja também

Publicidade
Bíblia Online Bíblia Online

Bíblia Online • Versão: 2026-06-16_06-50-08-