1 Waovu hukimbia wasipofuatiwa na mtu;
Bali wenye haki ni wajasiri kama simba.
2 Kwa sababu ya maasi ya nchi wakuu wake huwa wengi;
Bali kwa wenye ufahamu na maarifa hali ya nchi hudumishwa
3 Mtu mhitaji awaoneaye maskini,
Ni kama mvua ya dhoruba isiyosaza chakula.
4 Wao waiachao sheria huwasifu waovu;
Bali wao waishikao hushindana nao.
5 Watu waovu hawaelewi na haki;
Bali wamtafutao BWANA huelewa na zote.
6 Afadhali maskini aendaye katika unyofu wake,
Kuliko mpotovu wa njia angawa ni tajiri.
7 Yeye aishikaye sheria ni mwana mwenye hekima;
Bali aliye rafiki wa walafi humwaibisha babaye.
8 Yeye azidishaye mali yake kwa riba na faida,
Humkusanyia mtu awahurumiaye maskini.
9 Yeye aligeuzaye sikio lake asiisikie sheria,
Hata sala yake ni chukizo.
10 Kila mtu awapotezaye wenye haki katika njia mbaya,
Ataanguka katika rima lake mwenyewe;
Bali wakamilifu watarithi mema.
11 Mtu tajiri ana hekima machoni pake mwenyewe;
Bali maskini mwenye ufahamu humchunguza sana.
12 Wenye haki washindapo, uko utukufu mwingi;
Bali waovu waondokapo, watu hujificha.
13 Afichaye dhambi zake hatafanikiwa;
Bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema.
14 Mwanadamu mwenye kicho yu heri sikuzote;
Bali mshupavu wa moyo ataangukia madhara.
15 Kama simba angurumaye, na dubu mwenye njaa;
Ndivyo alivyo mtu mbaya awatawalaye maskini.
16 Mkuu aliyepungukiwa na akili huwaonea watu sana;
Bali achukiaye kutamani ataongeza siku zake.
17 Aliyelemewa na damu ya mtu
Atalikimbilia shimo; wala mtu asimzuie.
18 Aendaye kwa unyofu ataokolewa;
Bali mkaidi wa njia zake ataanguka mara.
19 Alimaye shamba lake atakuwa na chakula tele;
Bali afuataye mambo ya upuzi atapata umaskini wa kumtosha.
20 Mtu mwaminifu atakuwa na baraka tele;
Lakini afanyaye haraka kuwa tajiri hakosi ataadhibiwa.
21 Kupendelea watu si kwema;
Wala mtu kuasi kwa ajili ya kipande cha mkate.
22 Mwenye husuda afanya haraka kuwa tajiri;
Wala haufikiri uhitaji utakaomjia.
23 Amkemeaye mwenzake hatimaye atapata kibali;
Zaidi ya mtu ajipendekezaye kwa ulimi wake.
24 Aibaye mali ya babaye au mamaye, na kusema, Si kosa;
Mwana huyo ni rafiki wa mtu mharibifu.
25 Mwenye nafsi ya kutamani huchochea fitina;
Bali amtumainiye BWANA ataneemeshwa.
26 Mwenye kujitumainia moyo wake ni mjinga;
Bali yeye aendaye kwa busara ataokolewa.
27 Mwenye kuwagawia maskini hatahitaji kitu;
Bali afichaye macho yake atakuwa na laana nyingi.
28 Wasio haki wainukapo, wanadamu hujificha;
Bali waangamiapo, wenye haki huongezeka.