1 Moyo wa mfalme huwa katika mkono wa BWANA;
Kama mifereji ya maji huugeuza popote apendapo.
2 Kila njia ya mtu ni sawa machoni pake mwenyewe;
Bali BWANA huipima mioyo.
3 Kutenda haki na hukumu
Humpendeza BWANA kuliko kutoa sadaka.
4 Mwenye kiburi na moyo wa majivuno,
Taa yake ni dhambi.
5 Mawazo ya wenye bidii huuelekea utajiri tu;
Bali kila mwenye pupa huuelekea uhitaji.
6 Kupata akiba ya mali kwa ulimi wa uongo
Ni moshi upeperushwao; ni kutafuta mauti.
7 Jeuri ya wabaya itawaondolea mbali;
Kwa sababu wamekataa kutenda hukumu.
8 Njia yake aliyelemewa na dhambi imepotoka sana;
Bali mtu aliye safi, kazi yake ni sawasawa.
9 Ni afadhali kukaa katika pembe ya darini,
Kuliko katika nyumba pana pamoja na mwanamke mgomvi.
10 Nafsi ya mtu mbaya hutamani uovu;
Jirani yake hapati fadhili machoni pake.
11 Mwenye mzaha aadhibiwapo, mjinga hupata hekima;
Na mwenye hekima afundishwapo, hupokea maarifa.
12 Mwenye haki huitafakari nyumba ya mtu mbaya;
Jinsi wabaya waangushwavyo wakaangamia.
13 Azibaye masikio yake asisikie kilio cha maskini,
Yeye naye atalia, lakini hatasikiwa.
14 Kipawa cha siri hutuliza hasira;
Na rushwa bindoni humliza ghadhabu kali.
15 Ni furaha yao wenye haki kutenda hukumu;
Lakini ni uharibifu kwao watendao maovu.
16 Mtu aikosaye njia ya busara
Atakaa katika mkutano wao waliokufa.
17 Mtu apendaye anasa atakuwa maskini;
Apendaye mvinyo na mafuta hatakuwa tajiri.
18 Mtu asiye haki ni fidia ya wenye haki;
Naye afanyaye hila ni badala ya watu wa adili.
19 Ni afadhali kukaa katika nchi ya nyika;
Kuliko na mwanamke mgomvi, mchokozi.
20 Kuna hazina ya thamani na mafuta katika maskani ya mwenye hekima;
Bali mwanadamu aliye mpumbavu huyameza.
21 Aandamaye haki na fadhili,
Ataona uhai na haki na heshima.
22 Mwenye hekima huupandia mji wao wenye nguvu;
Na kuziangusha nguvu za tumaini lao.
23 Mtu azuiaye kinywa chake na ulimi wake,
Atajilinda nafsi yake na taabu.
24 Mwenye kiburi na kutakabari, jina lake ni mbishi;
Hutenda mambo katika majivuno ya kiburi chake.
25 Matakwa yake mtu mvivu humwua,
Kwa maana mikono yake hukataa kufanya kazi.
26 Kuna atamaniye kwa choyo mchana kutwa;
Bali mwenye haki hutoa wala hanyimi.
27 Sadaka ya wasio haki ni chukizo;
Si zaidi sana ailetapo mwenye nia mbaya!
28 Shahidi wa uongo atapotea;
Bali mtu asikiaye atasema maneno yadumuyo.
29 Asiye haki huufanya uso wake kuwa mgumu;
Bali mtu mnyofu huzifikiri njia zake.
30 Hapana hekima, wala ufahamu,
Wala shauri, juu ya BWANA.
31 Farasi huwekwa tayari kwa siku ya vita;
Lakini BWANA ndiye aletaye wokovu.