Publicidade

Provérbios 17

1 Afadhali mego kavu pamoja na utulivu,

Kuliko nyumba yenye karamu nyingi pamoja na magomvi.

2 Mtumwa atendaye kwa busara atamtawala mwana atendaye mambo ya aibu;

Tena atapata sehemu ya urithi kati ya ndugu.

3 Zab 26:2;Mit 27:21;Yer 17:10;Mal 3:3 Kalibu ni kwa fedha, na tanuri kwa dhahabu;

Bali BWANA huijaribu mioyo.

4 Mtenda mabaya husikiliza midomo ya uovu;

Na mwongo hutega sikio lake kusikiliza ulimi wa madhara.

5 Ayu 31:29;Mit 24:17;Oba 1:12 Amchekaye maskini humtukana Muumba wake;

Naye aufurahiaye msiba hatakosa adhabu.

6 Wana wa wana ndio taji la wazee,

Na utukufu wa watoto ni baba zao.

7 Maneno mazuri hayapendezi kinywani mwa mpumbavu;

Sembuse midomo ya uongo kinywani mwa mkuu.

8 Mwa 39:21;Dan 6:3 Kipawa ni kama kito cha thamani machoni pake yeye aliye nacho;

Kila kigeukapo hufanikiwa.

9 Afunikaye kosa hutafuta kupendwa;

Bali yeye afichuaye siri hutenga rafiki.

10 Lawama hupenya moyoni mwa mwenye ufahamu,

Kuliko mapigo mia moyoni mwa mpumbavu.

11 Mtu mwovu hataki neno ila kuasi tu;

Kwa hiyo mjumbe mkali atatumwa kwake.

12 Afadhali mtu akutwe na dubu jike aliyenyang’anywa watoto wake,

Kuliko na mpumbavu katika upumbavu wake.

13 Yer 18:20;Rum 12:17;1 The 5:15 Yeye arudishaye mabaya badala ya mema,

Mabaya hayataondoka nyumbani mwake.

14 Mit 20:3;Mdo 6:1;Rum 12:18;1 The 4:11 Mwanzo wa ugomvi ni kama kutoboa penye maji;

Basi acheni ugomvi kabla haujafurika.

15 Kut 23:7;Isa 5:23 Yeye asemaye kwamba asiye haki ana haki;

naye asemaye kwamba mwenye haki hana haki;

Hao wote wawili ni chukizo kwa BWANA.

16 Nini maana yake, mpumbavu kuwa na fedha mkononi mwake ya kununulia hekima,

Ikiwa hana moyo wa ufahamu?

17 Rafiki hupenda sikuzote;

Na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.

18 Asiye na hekima hupeana mkono na mtu;

Na kuwa mdhamini wa mtu mwingine.

19 Apendaye ugomvi hupenda dhambi;

Auinuaye sana mlango wake hutafuta uharibifu.

20 Mtu mwenye moyo wa ukaidi hatapata mema;

Na mwenye ulimi wa upotovu huanguka katika misiba.

21 Azaaye mpumbavu ni kwa huzuni yake mwenyewe;

Wala baba wa mpumbavu hana furaha.

22 Moyo uliochangamka ni dawa nzuri;

Bali roho iliyopondeka huikausha mifupa.

23 Kut 23:8 Asiye haki hutoa rushwa kifuani,

Ili kuzipotosha njia za hukumu.

24 Mhu 2:14 Hekima huwa machoni pake mwenye ufahamu;

Bali macho ya mpumbavu huwa katika ncha za dunia.

25 Mwana mpumbavu ni huzuni kwa babaye,

Na uchungu kwa mamaye aliyemzaa.

26 Tena kumwadhibu mwenye haki si vizuri;

Wala si vyema kuwapiga wakuu kwa unyofu wao.

27 Yak 1:19 Azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa;

Na mwenye roho ya utulivu ana busara.

28 Hata mpumbavu akinyamaza, huhesabiwa hekima;

Akifumba midomo yake, huhesabiwa ufahamu.

Veja também

Bíblia Online Bíblia Online

Bíblia Online • Versão: 2026-07-04_23-13-58-