Publicidade

Isaías 18

Utabiri juu ya Kushi

1 Ole wa nchi ya uvumi wa mabawa,

Iliyoko mbali kupita mito ya Kushi;

2 Ipelekayo wajumbe wake kwa njia ya bahari,

Na katika vyombo vya manyasi juu ya maji.

Nendeni, wajumbe wepesi, kwa watu warefu, laini;

Watu watishao tangu mwanzo wao hata sasa;

Taifa la wenye nguvu, wakanyagao watu,

Ambao mito inakata nchi yao.

3 Enyi watu mkaao katika ulimwengu wote, na wenyeji wa dunia, bendera ikiinuliwa milimani, angalieni; na wakipiga tarumbeta, sikieni. 4 Maana BWANA ameniambia hivi, Mimi nitatulia, na kuangalia katika makazi yangu, kama wakati wa mwangaza mweupe wa jua kali, mfano wa wingu la umande katika joto la mavuno. 5 Maana kabla ya mavuno, maua yaangukapo, na maua yakawa zabibu zianzazo kuiva, ndipo atakapoyakata matawi kwa miundu, na kuviondoa vitawi vilivyopanuka na kuvikata. 6 Wote pamoja wataachiwa ndege wakali wa milimani, na wanyama wa nchi; ndege wakali watakaa juu yao wakati wa jua, na wanyama wote wa nchi watakaa juu yao wakati wa baridi. 7 Wakati huo BWANA wa majeshi ataletewa hidaya na watu warefu, laini;

Watu watishao tangu mwanzo wao hata sasa;

Taifa la wenye nguvu, wakanyagao watu,

Ambao mito inagawanya nchi yao;

Mpaka mahali pa jina la BWANA wa majeshi, mlima Sayuni.

Veja também

Publicidade
Bíblia Online Bíblia Online

Bíblia Online • Versão: 2026-06-16_18-40-07-