1 Kwa ajili ya Sayuni sitanyamaza, na kwa ajili ya Yerusalemu sitatulia, hata haki yake itakapotokea kama mwangaza, na wokovu wake kama taa iwakayo. 2 Na mataifa wataiona haki yako, na wafalme wote watauona utukufu wako; nawe utaitwa jina jipya, litakalotajwa na kinywa cha BWANA. 3 Nawe utakuwa taji la uzuri katika mkono wa BWANA, na kilemba cha kifalme mkononi mwa Mungu wako. 4 Hutaitwa tena Aliyeachwa, wala nchi yako haitaitwa tena, Ukiwa; bali utaitwa Hefziba; na nchi yako Beula; kwa kuwa BWANA anakufurahia, na nchi yako itaolewa. 5 Maana kama vile kijana amwoavyo mwanamwali, ndivyo wana wako watakavyokuoa wewe; na kama vile bwana arusi amfurahiavyo bibi arusi, ndivyo Mungu wako atakavyokufurahia wewe.
6 Nimeweka walinzi juu ya kuta zako, Ee Yerusalemu; hawatanyamaza mchana wala usiku; ninyi wenye kumkumbusha BWANA, msiwe na kimya; 7 wala msimwache akae kimya, mpaka atakapouimarisha Yerusalemu, na kuufanya usifike kote duniani. 8 BWANA ameapa kwa mkono wake wa kulia, na kwa mkono wa nguvu zake, Hakika sitawapa adui zako nafaka yako tena kuwa chakula chao; wala wageni hawatakunywa divai yako, uliyoifanyia kazi. 9 Lakini walioivuna, ndio watakaoila, na kumhimidi BWANA; na walioichuma, ndio watakaoinywa, ndani ya nyua za patakatifu pangu.
10 Piteni, piteni, katika malango;
Itengenezeni njia ya watu;
Tutieni, tutieni barabara; toeni mawe yake;
Twekeni bendera kwa ajili ya makabila ya watu.
11 Tazama, BWANA ametangaza habari mpaka mwisho wa dunia,
Mwambieni binti Sayuni,
Tazama, wokovu wako unakuja;
Tazama, thawabu yake iko pamoja naye,
Na malipo yake yako mbele zake.
12 Nao watawaita, Watu watakatifu,
Waliokombolewa na BWANA;
Nawe utaitwa, Aliyetafutwa,
Mji usioachwa.