1 Ni nani aliyesadiki habari tuliyoileta?
Na mkono wa BWANA amefunuliwa nani?
2 Maana alikuwa mbele zake kama mche mwororo,
Na kama mzizi katika nchi kavu;
Yeye hana umbo wala uzuri;
Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani.
3 Alidharauliwa na kukataliwa na watu;
Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko;
Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao,
Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu.
4 Hakika ameyachukua masikitiko yetu,
Amejitwika huzuni zetu;
Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa,
Amepigwa na Mungu, na kuteswa.
5 Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu,
Alichubuliwa kwa maovu yetu;
Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake,
Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.
6 Sisi sote kama kondoo tumepotea;
Kila mmoja wetu amegeukia njia yake mwenyewe;
Na BWANA ameweka juu yake
Maovu yetu sisi sote.
7 Alionewa, lakini alinyenyekea,
Wala hakufunua kinywa chake;
Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni,
Na kama vile kondoo anyamazavyo
Mbele yao wakatao manyoya yake;
Naam, hakufunua kinywa chake.
8 Kwa kuonewa na kuhukumiwa aliondolewa;
Na maisha yake ni nani angeyajali?
Maana amekatiliwa mbali na nchi ya walio hai;
Alipigwa kwa sababu ya makosa ya watu wangu.
9 Wakamfanyia kaburi pamoja na wabaya;
Na pamoja na matajiri katika kufa kwake;
Ingawa hakutenda jeuri,
Wala hapakuwa na hila kinywani mwake.
10 Lakini BWANA aliridhika kumchubua;
Amemhuzunisha;
Utakapofanya nafsi yake kuwa dhabihu kwa dhambi,
Ataona uzao wake, ataishi siku nyingi,
Na mapenzi ya BWANA yatafanikiwa mkononi mwake;
11 Ataona mazao ya taabu ya nafsi yake, na kuridhika.
Kwa maarifa yake mtumishi wangu mwenye haki
Atawafanya wengi kuwa wenye haki;
Naye atayachukua maovu yao.
12 Kwa hiyo nitamgawia sehemu pamoja na wakuu,
Naye atagawana nyara pamoja nao walio hodari;
Kwa sababu alimwaga nafsi yake hata kufa,
Akahesabiwa pamoja na hao wakosao.
Walakini alichukua dhambi za watu wengi,
Na kuwaombea wakosaji.