Sofari anena: Hatia ya Ayubu yastahili adhabu
1 Ndipo Sofari Mnaamathi akajibu, na kusema,
2 Je! Huu wingi wa maneno usijibiwe?
Na mtu aliyejaa maneno, je! Ahesabiwe kuwa na haki?
3 Je! Majivuno yako yawanyamazishe watu wawe kimya?
Nawe hapo ufanyapo dhihaka, je! Hapana mtu atakayekutahayarisha?
4 Ayu 6:10;1 Pet 3:15 Kwa kuwa wewe wasema, Mafunzo yangu ni safi,
Nami ni safi machoni pako.
5 Lakini, laiti Mungu angenena,
Na kuifunua midomo yake juu yako;
6 Omb 3:22 Tena akuoneshe hizo siri za hekima,
Ya kuwa hufanikiwa katika kuyatimiza makusudi yake!
Ujue basi ya kuwa Mungu akuachilia katika uovu wako.
7 Ayu 5:9;Mhu 3:11;Isa 40:28;Mt 11:27;Rum 11:33;Efe 3:8 Je! Wewe waweza kuuvumbua ukuu wa Mungu?
Waweza kuufikia upeo wa huyo Mwenyezi?
8 Ni juu mno kama mbingu; waweza kufanya nini wewe?
Ni wenye kina kuliko kuzimuni; waweza kujua nini wewe?
9 Cheo chake ni kirefu kuliko dunia,
Ni kipana zaidi ya bahari.
10 Yeye akipita, na kufunga watu,
Na kuwaita hukumuni, ni nani basi awezaye kumzuia?
11 Zab 10:11 Kwa kuwa yeye awajua watu baradhuli;
Anapouona uovu, je; hatauangalia?
12 Lakini mpumbavu aweza kupata ufahamu,
Ingawa mwanadamu huzaliwa kama mtoto wa punda mwitu.
13 1 Sam 7:3;Zab 78:8;143:6 Wewe ukiuweka moyo wako kwa uelekevu,
Na kumnyoshea mikono yako;
14 Ikiwa una uovu mkononi mwako, uweke mbali nawe,
Wala usikubali upuzi kukaa hemani mwako;
15 Mwa 4:5;Ayu 22:26;Zab 119:6;1 Tim 2:8;1 Yoh 3:21 Hakika ndipo utakapopata kuinua uso pasipo ila;
Naam, utathibitika, wala hutakuwa na hofu;
16 Kwa kuwa utasahau mateso yako;
Utayakumbuka kama maji yaliyokwisha pita;
17 Na maisha yako yatakuwa meupe kuliko adhuhuri;
Giza lake litakuwa kama alfajiri.
18 Nawe utakuwa salama, kwa sababu kuna matumaini;
Naam, utatafutatafuta kando yako, na kupumzika salama.
19 Tena utalala, wala hapana atakayekutia hofu;
Naam, wengi watakutafuta uso wako.
20 Lakini macho ya waovu yataingia kiwi,
Nao hawatakuwa na njia ya kukimbilia,
Na matumaini yao yatakuwa ni kutoa roho.