Publicidade

Jó 17

Ayubu aomba apate faraja

1 Roho yangu imezimia, siku zangu zimekoma,

Kaburi i tayari kunipokea.

2 Ni kweli wako kwangu wenye kufanya dhihaka,

Jicho langu hukaa katika kunifanyia uchungu kwao.

3 Nipe rehani basi, uwe dhamana kwa ajili yangu kwako wewe mwenyewe;

Kuna nani atakayeniwekea dhamana?

4 Kwa kuwa umezifumba akili zao ufahamu;

Kwa hiyo hutawaacha wanishinde.

5 Awafitiniye rafiki zake wawe mawindo,

Hata macho ya watoto wake yataingia kiwi.

6 Amenifanya niwe mithali kwa watu;

Nimekuwa mwenye kuchukiwa kwa wazi.

7 Jicho langu nalo limekuwa giza kwa sababu ya majonzi,

Na viungo vyangu vyote vimekuwa kama kivuli.

8 Walekevu watayastaajabia hayo,

Na asiye na hatia atajiamsha juu ya mpotovu.

9 Lakini mwenye haki ataishika njia yake,

Naye mwenye mikono safi atazidi kupata nguvu.

10 Lakini rudini; ninyi nyote, njoni sasa;

Wala sitampata mtu mwenye hekima kati yenu.

11 Siku zangu zimepita, makusudi yangu yamevunjika,

Hata hayo niliyo nayo moyoni mwangu.

12 Wabadili usiku kuwa mchana;

Wasema, Mwanga u karibu kwa sababu ya giza.

13 Nikitazamia kuzimu kuwa nyumba yangu;

Nikitandika malazi yangu gizani;

14 Ikiwa nimeuita uharibifu, Wewe u baba yangu;

Na kuliambia buu, Wewe u mama yangu, na dada yangu;

15 Basi, tumaini langu liko wapi?

Na tumaini langu, ni nani atakayeliona?

16 Litashuka kwenye makomeo ya kuzimu,

Itakapokuwapo raha mavumbini.

Veja também

Publicidade
Bíblia Online Bíblia Online

Bíblia Online • Versão: 2026-06-19_11-20-24-