1 Roho yangu imezimia, siku zangu zimekoma,
Kaburi i tayari kunipokea.
2 Ni kweli wako kwangu wenye kufanya dhihaka,
Jicho langu hukaa katika kunifanyia uchungu kwao.
3 Nipe rehani basi, uwe dhamana kwa ajili yangu kwako wewe mwenyewe;
Kuna nani atakayeniwekea dhamana?
4 Kwa kuwa umezifumba akili zao ufahamu;
Kwa hiyo hutawaacha wanishinde.
5 Awafitiniye rafiki zake wawe mawindo,
Hata macho ya watoto wake yataingia kiwi.
6 Amenifanya niwe mithali kwa watu;
Nimekuwa mwenye kuchukiwa kwa wazi.
7 Jicho langu nalo limekuwa giza kwa sababu ya majonzi,
Na viungo vyangu vyote vimekuwa kama kivuli.
8 Walekevu watayastaajabia hayo,
Na asiye na hatia atajiamsha juu ya mpotovu.
9 Lakini mwenye haki ataishika njia yake,
Naye mwenye mikono safi atazidi kupata nguvu.
10 Lakini rudini; ninyi nyote, njoni sasa;
Wala sitampata mtu mwenye hekima kati yenu.
11 Siku zangu zimepita, makusudi yangu yamevunjika,
Hata hayo niliyo nayo moyoni mwangu.
12 Wabadili usiku kuwa mchana;
Wasema, Mwanga u karibu kwa sababu ya giza.
13 Nikitazamia kuzimu kuwa nyumba yangu;
Nikitandika malazi yangu gizani;
14 Ikiwa nimeuita uharibifu, Wewe u baba yangu;
Na kuliambia buu, Wewe u mama yangu, na dada yangu;
15 Basi, tumaini langu liko wapi?
Na tumaini langu, ni nani atakayeliona?
16 Litashuka kwenye makomeo ya kuzimu,
Itakapokuwapo raha mavumbini.