1 Ndipo Ayubu akajibu, na kusema,
2 Hata leo malalamiko yangu yana uchungu;
Pigo langu ni zito zaidi ya kuugua kwangu.
3 Laiti ningejua mahali niwezapo kumwona,
Nifike hata hapo anapokaa!
4 Ningeiweka kesi yangu mbele yake,
Na kukijaza kinywa changu hoja.
5 Ningeyajua maneno atakayonijibu,
Na kuelewa hayo atakayoniambia.
6 Je! Angeshindana nami kwa ukuu wa uwezo wake?
La, lakini angenisikiliza.
7 Hapo waelekevu wangepata kuhojiana naye;
Basi hivyo ningeachiliwa na mwamuzi wangu milele.
8 Tazama, naenda mbele, wala hayuko;
Narudi nyuma, lakini siwezi kumwona;
9 Na mkono wa kushoto, afanyapo kazi, lakini siwezi kumwona;
Hujificha upande wa kulia, hata nisimwone.
10 Lakini yeye aijua njia niendeayo;
Akisha kunijaribu, nitatoka kama dhahabu.
11 Mguu wangu umeshikamana sana na hatua zake;
Njia yake nimeishika, wala sikukengeuka.
12 Sikurudi nyuma kuiacha amri ya midomo yake;
Nimeyatunza maneno ya kinywa chake zaidi ya riziki yangu,
13 Lakini yeye ni mmoja, ni nani awezaye kumgeuza?
Tena nafsi yake ilitakalo, ndilo afanyalo.
14 Kwani yeye hulitimiliza hilo nililoamriwa;
Tena mambo mengi kama hayo ya pamoja naye.
15 Kwa hiyo naona taabu mbele ya uso wake;
Nitakapofikiri, namwogopa.
16 Kwa maana Mungu ameufanya moyo wangu kuzimia,
Naye Mwenyezi amenitaabisha;
17 Maana sikufadhaishwa kwa sababu ya giza,
Wala kwa sababu giza kuu limenifunika uso.