Publicidade

Salmos 29

Sauti Ya Bwana Wakati Wa Dhoruba
Zaburi ya Daudi.

1 Mpeni Bwana, enyi mashujaa,

mpeni Bwana utukufu na nguvu.

2 Mpeni Bwana utukufu unaostahili jina lake;

mwabuduni Bwana katika uzuri wa utakatifu wake.

3 Sauti ya Bwana iko juu ya maji;

Mungu wa utukufu hupiga radi,

Bwana hupiga radi juu ya maji makuu.

4 Sauti ya Bwana ina nguvu;

sauti ya Bwana ni tukufu.

5 Sauti ya Bwana huvunja mierezi;

Bwana huvunja vipande vipande

mierezi ya Lebanoni.

6 Hufanya Lebanoni irukaruke kama ndama,

Sirioni urukaruke kama mwana nyati.

7 Sauti ya Bwana hupiga kwa miali

ya umeme wa radi.

8 Sauti ya Bwana hutikisa jangwa;

Bwana hutikisa Jangwa la Kadeshi.

9 Sauti ya Bwana huzalisha ayala,

na huuacha msitu wazi.

Hekaluni mwake wote wasema,

"Utukufu!"

10 Bwana huketi akiwa ametawazwa juu ya gharika;

Bwana ametawazwa kuwa Mfalme milele.

11 Bwana huwapa watu wake nguvu;

Bwana huwabariki watu wake kwa kuwapa amani.

Veja também

Publicidade
Bíblia Online Bíblia Online

Bíblia Online • Versão: 2026-06-15_21-32-39-