Wimbo wa Daudi wa ushindi
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi mtumishi wa Mwenyezi Mungu aliyomwimbia Mwenyezi Mungu alipomwokoa mikononi mwa adui zake wote, na pia mkononi mwa Sauli. Alisema hivi:
1 Nakupenda wewe, Ee Mwenyezi Mungu,
nguvu yangu.
2 Mwenyezi Mungu ni mwamba wangu,
ngome yangu na mwokozi wangu;
Mungu wangu ni mwamba wangu,
ninayemkimbilia.
Yeye ni ngao yangu na pembe ya wokovu wangu,
ngome yangu.
3 Ninamwita Mwenyezi Mungu anayestahili kusifiwa,
nami ninaokolewa kutoka kwa adui zangu.