Publicidade

Salmos 96

Mwenyezi Mungu Mfalme mkuu

1 Mwimbieni Mwenyezi Mungu wimbo mpya;

mwimbieni Mwenyezi Mungu dunia yote.

2 Mwimbieni Mwenyezi Mungu, lisifuni jina lake;

tangazeni wokovu wake siku baada ya siku.

3 Tangazeni utukufu wake katika mataifa,

matendo yake ya ajabu miongoni mwa mataifa yote.

4 Kwa kuwa Mwenyezi Mungu ni mkuu mwenye kustahili kusifiwa kuliko wote;

yeye ni wa kuogopwa kuliko miungu yote.

5 Kwa maana miungu yote ya mataifa ni sanamu,

lakini Mwenyezi Mungu aliziumba mbingu.

6 Fahari na enzi viko mbele yake;

nguvu na utukufu vimo patakatifu pake.

7 Mpeni Mwenyezi Mungu, enyi jamaa za mataifa,

mpeni Mwenyezi Mungu utukufu na nguvu.

8 Mpeni Mwenyezi Mungu utukufu unaostahili jina lake;

leteni sadaka na mje katika nyua zake.

9 Mwabuduni Mwenyezi Mungu katika uzuri wa utakatifu wake;

dunia yote na itetemeke mbele zake.

10 Semeni katika mataifa kwamba, "Mwenyezi Mungu anatawala."

Ulimwengu ameuweka imara, hauwezi kusogezwa;

atawahukumu watu kwa uadilifu.

11 Mbingu na zishangilie, nchi na ifurahi;

bahari na ivume, na vyote vilivyo ndani yake;

12 mashamba na yashangilie,

pamoja na vyote vilivyomo.

Kisha miti yote ya msituni itaimba kwa furaha;

13 itaimba mbele za Mwenyezi Mungu kwa maana anakuja,

anakuja kuihukumu dunia.

Ataihukumu dunia kwa haki,

na mataifa katika kweli yake.

Veja também

Publicidade
Bíblia Online Bíblia Online

Bíblia Online • Versão: 2026-06-16_06-50-08-