Publicidade

Salmos 29

Sauti ya Mwenyezi Mungu wakati wa dhoruba
Zaburi ya Daudi.

1 Mpeni Mwenyezi Mungu, enyi mashujaa,

mpeni Mwenyezi Mungu utukufu na nguvu.

2 Mpeni Mwenyezi Mungu utukufu unaostahili jina lake;

mwabuduni Mwenyezi Mungu katika uzuri wa utakatifu wake.

3 Sauti ya Mwenyezi Mungu iko juu ya maji;

Mungu wa utukufu hupiga radi,

Mwenyezi Mungu hupiga radi juu ya maji makuu.

4 Sauti ya Mwenyezi Mungu ina nguvu;

sauti ya Mwenyezi Mungu ni tukufu.

5 Sauti ya Mwenyezi Mungu huvunja mierezi;

Mwenyezi Mungu huvunja vipande vipande

mierezi ya Lebanoni.

6 Hufanya Lebanoni irukaruke kama ndama,

Sirioni urukaruke kama mwana nyati.

7 Sauti ya Mwenyezi Mungu hupiga

kwa miali ya radi.

8 Sauti ya Mwenyezi Mungu hutikisa jangwa;

Mwenyezi Mungu hutikisa Jangwa la Kadeshi.

9 Sauti ya Mwenyezi Mungu huzalisha ayala,

na huuacha msitu wazi.

Hekaluni mwake wote wasema,

"Utukufu!"

10 Mwenyezi Mungu huketi akiwa ametawazwa juu ya gharika;

Mwenyezi Mungu ametawazwa kuwa Mfalme milele.

11 Mwenyezi Mungu huwapa watu wake nguvu;

Mwenyezi Mungu huwabariki watu wake kwa kuwapa amani.

Veja também

Publicidade
Bíblia Online Bíblia Online

Bíblia Online • Versão: 2026-06-16_06-50-08-