Publicidade

Salmos 46

Mwenyezi Mungu yuko pamoja nasi
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya wana wa Kora. Mtindo wa alamothi.

1 Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu,

msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.

2 Kwa hiyo hatutaogopa, hata kama dunia ikiondolewa,

na milima ianguke kilindini cha bahari,

3 hata maji yake yakinguruma na kuumuka,

na milima itetemeke kwa mawimbi yake.

4 Kuna mto ambao vijito vyake vinaufurahisha mji wa Mungu,

mahali patakatifu ambako Aliye Juu Sana anaishi.

5 Mungu yuko katikati yake, hautaanguka,

Mungu atausaidia asubuhi na mapema.

6 Mataifa yanafanya ghasia, falme zinaanguka,

yeye hupaza sauti yake, dunia ikayeyuka.

7 Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni

yu pamoja nasi;

Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.

8 Njooni mkaone kazi za Mwenyezi Mungu

jinsi alivyofanya ukiwa katika nchi.

9 Anakomesha vita hata miisho ya dunia,

anakata upinde na kuvunjavunja mkuki,

anateketeza ngao kwa moto.

10 "Tulieni, mjue kwamba mimi ndimi Mungu;

nitatukuzwa katikati ya mataifa,

nitatukuzwa katika dunia."

11 Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni

yu pamoja nasi;

Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.

Veja também

Publicidade
Bíblia Online Bíblia Online

Bíblia Online • Versão: 2026-06-16_18-40-07-