Publicidade

Salmos 12

Ombi la msaada wakati wa dhiki
Kwa mwimbishaji: kwa kufuata Sheminithi. Zaburi ya Daudi.

1 Tuokoe, ee BWANA, maana hamna tena amchaye Mungu

Maana waaminifu wametoweka katika wanadamu.

2 Husemezana yasiyofaa kila mtu na mwenziwe,

Wenye midomo ya kujipendekeza;

Husemezana kwa mioyo ya unafiki;

3 BWANA ataikata midomo yote ya kujipendekeza,

Na ulimi unenao maneno ya kiburi;

4 Waliosema, Kwa ndimi zetu tutashinda;

Midomo yetu ni yetu wenyewe,

Ni nani aliye bwana juu yetu?

5 Kwa ajili ya kuonewa kwao wanyonge,

Kwa ajili ya kuugua kwao wahitaji,

Sasa nitasimama, asema BWANA,

Nitamweka salama yeye wanayemfyonya.

6 Maneno ya BWANA ni maneno safi,

Ni fedha iliyojaribiwa kalibuni juu ya nchi;

Iliyosafishwa mara saba.

7 Wewe, BWANA, ndiwe utakayetuhifadhi,

Utatulinda na kizazi hiki milele.

8 Wasio haki hutembea pande zote,

Huku ufisadi ukitukuka kati ya wanadamu.

Veja também

Publicidade
Bíblia Online Bíblia Online

Bíblia Online • Versão: 2026-06-16_06-50-08-