1 BWANA, usinikemee kwa hasira yako,
Wala usinirudi kwa ghadhabu yako.
2 BWANA, unifadhili, maana ninanyauka;
BWANA, uniponye, mifupa yangu imefadhaika.
3 Na nafsi yangu imefadhaika sana;
Na Wewe, BWANA, hadi lini?
4 BWANA urudi, uniopoe nafsi yangu,
Uniokoe kwa ajili ya fadhili zako.
5 Maana mautini hapana kumbukumbu lako;
Katika kuzimu ni nani atakayekushukuru?
6 Nimechoka kwa kuugua kwangu;
Kila usiku nakibubujikia kitanda changu;
Nililowesha godoro langu kwa machozi yangu.
7 Macho yangu yameharibika kwa masumbufu,
Na kuchakaa kwa sababu yao wanaoniudhi.
8 Ondokeni kwangu, ninyi nyote mtendao uovu;
Kwa kuwa BWANA ameisikia sauti ya kilio changu.
9 BWANA ameisikia dua yangu;
BWANA atayatakabali maombi yangu.
10 Adui zangu wote wataaibika na kufadhaika,
Watarudi nyuma, kwa ghafla wataaibika.