1 Ee BWANA, uisikie sala yangu, uzisikilize dua zangu Unijibu Kwa uaminifu wako,
Unijibu kwa haki yako.
2 Wala usimhukumu mtumishi wako,
Maana kwako hakuna aliye hai mwenye haki.
3 Maana adui ameifuatia nafsi yangu,
Ameutupa chini uzima wangu.
Amenikalisha mahali penye giza,
Kama watu waliokufa zamani.
4 Na roho yangu imezimia ndani yangu,
Moyo wangu ndani yangu umeshtuka.
5 Nimezikumbuka siku za kale,
Nimeyatafakari matendo yako yote,
Naziwaza kazi za mikono yako.
6 Nakunyoshea mikono yangu;
Nafsi yangu inakuonea kiu kama nchi kame.
7 Ee BWANA, unijibu hima, roho yangu imelegea;
Usinifiche uso wako,
Nisifanane nao washukao shimoni.
8 Uniwezeshe kusikia fadhili zako asubuhi,
Kwa maana nimekutumaini Wewe.
Unifundishe njia nitakayoiendea,
Kwa maana ninakuinulia nafsi yangu.
9 Ee BWANA, uniponye kutoka kwa adui zangu;
Nimekukimbilia Wewe, unifiche.
10 Unifundishe kuyatenda mapenzi yako,
Kwa maana ndiwe Mungu wangu;
Roho yako mwema aniongoze katika njia iliyo sawa,
11 Ee BWANA, uniponye kwa ajili ya jina lako,
Kwa haki yako unitoe roho yangu taabuni;
12 Kwa fadhili zako utawakatilia mbali adui zangu;
Na kuwaangamiza wote wanitesao nafsi,
Kwa maana mimi ni mtumishi wako.