1 Ee BWANA, nitakuita Ewe, mwamba wangu,
Usiwe kwangu kama kiziwi.
Nisije nikafanana nao washukao shimoni,
Ikiwa umeninyamalia.
2 Uisikie sauti ya dua yangu nikuombapo,
Nikipainulia patakatifu pako mikono yangu.
3 Usinikokote pamoja na wasio haki,
Wala pamoja na watenda maovu.
Wawaambiao jirani zao maneno ya amani,
Lakini mioyoni mwao mna madhara.
4 Uwape sawasawa na vitendo vyao,
Na kwa kadiri ya uovu wa matendo yao,
Uwape sawasawa na kazi ya mikono yao,
Uwalipe kile wanachostahili.
5 Maana hawazifahamu kazi za BWANA,
Wala matendo ya mikono yake,
Atawavunja wala hatawajenga tena;
6 Na ahimidiwe BWANA.
Maana ameisikia sauti ya dua yangu;
7 BWANA ni nguvu zangu na ngao yangu.
Moyo wangu umemtumaini,
Nami nimesaidiwa;
Basi, moyo wangu unashangilia,
Na kwa wimbo wangu nitamshukuru.
8 BWANA ni nguvu za watu wake,
Naye ni ngome ya wokovu kwa masihi wake.
9 Uwaokoe watu wako, uubariki urithi wako,
Uwachunge, uwachukue milele.