1 Mungu, unirehemu, maana yuko atakaye kunimeza,
Mchana kutwa ananionea akileta vita.
2 Adui zangu wanataka kunimeza mchana kutwa,
Maana ni wengi wanaonipiga vita.
3 Siku ya hofu yangu nitakutumaini Wewe;
4 Kwa msaada wa MUNGU nitalisifu neno lake.
Nimemtumaini Mungu, sitaogopa;
Mwenye mwili atanitenda nini?
5 Mchana kutwa wanapotosha maneno yangu,
Mawazo yao yote ni juu yangu kunitakia mabaya.
6 Hukutanika, hujificha, huziangalia nyayo zangu,
Kwa kuwa waliniotea ili waniue.
7 Je! Wataokoka kwa uovu wao?
Ee Mungu, uwaangamize kwa hasira yako.
8 Umehesabu kutangatanga kwangu;
Uyatie machozi yangu katika chupa yako;
(Je! Hayamo katika kitabu chako?)
9 Ndipo adui zangu watarudi nyuma siku ile niitapo.
Neno hili najua kuwa MUNGU yu upande wangu;
10 Kwa msaada wa MUNGU nitalisifu neno lake.
Kwa msaada wa BWANA nitalisifu neno lake.
11 Nimemtumaini Mungu, sitaogopa;
Mwanadamu atanitenda nini?
12 Ee Mungu, nadhiri zako ziko juu yangu;
Nitakutolea dhabihu za kushukuru.
13 Maana umeniponya nafsi yangu na mauti;
Je! Hukuizuia miguu yangu isianguke?
Ili niende mbele za Mungu
Katika nuru ya walio hai.