Kushutumiwa kwa wasiomwamini Mungu
Kwa mwimbishaji: kwa mtindo wa Mahalathi. Utenzi wa Daudi.
1 Mpumbavu husema moyoni, Hakuna Mungu;
Ni wafisadi, na wametenda mambo ya kuchukiza,
Hakuna atendaye mema.
2 Toka mbinguni MUNGU aliwachungulia wanadamu,
Aone kama yuko mtu mwenye hekima,
Amtafutaye Mungu.
3 Kila mtu amepotoka, wameoza wote pamoja,
Hakuna atendaye mema,
La! Hata mmoja.
4 Je! Wafanyao maovu hawajui?
Walao watu wangu kama walavyo mkate,
Hawakumwita MUNGU.
5 Hapo waliingiwa na hofu pasipokuwapo hofu,
Maana Mungu ameitawanya mifupa yake aliyekuhusuru.
Umewatia aibu,
Kwa sababu MUNGU amewadharau.
6 Laiti wokovu wa Israeli utoke katika Sayuni!
MUNGU awarudishapo wafungwa wa watu wake;
Yakobo atashangilia,
Israeli atafurahi.