1 BWANA, umeiridhia nchi yako,
Umewarejesha mateka wa Yakobo.
2 Umeusamehe uovu wa watu wako,
Umezisitiri hatia zao zote.
3 Umeiondoa ghadhabu yako yote,
Umerudi na kuuacha ukali wa hasira yako.
4 Mungu wa wokovu wetu, uturudishe,
Uikomeshe hasira uliyo nayo juu yetu.
5 Je! Utatufanyia hasira hata milele?
Utadumisha ghadhabu kizazi hadi kizazi?
6 Je! Hutaki kurudi na kutuhuisha,
Ili watu wako wakufurahie?
7 Ee BWANA, utuoneshe rehema zako,
Utupe wokovu wako.
8 Na nisikie atakavyosema Mungu BWANA,
Maana atawaambia watu wake amani,
Naam, na watauwa wake pia,
Bali wasiurudie upumbavu tena.
9 Hakika wokovu wake uko karibu na wamchao,
Ndipo utukufu wake ukae katika nchi yetu.
10 Fadhili na kweli zitakutana,
Haki na amani zitakumbatiana.
11 Kweli itachipuka katika nchi,
Haki itachungulia kutoka mbinguni.
12 Naam, BWANA atatoa kilicho chema,
Na nchi yetu itatoa mazao yake.
13 Haki itakwenda mbele zake,
Na kuzitayarishia hatua zake mapito.