1 Nafsi yangu yamngoja Mungu peke yake kwa utulivu,
Wokovu wangu hutoka kwake.
2 Yeye tu ndiye mwamba wangu na wokovu wangu,
Ngome yangu, sitatikisika.
3 Hadi lini mtamshambulia mtu,
Mpate kumwua ninyi nyote pamoja?
Kama ukuta unaoinama,
Kama ua ulio tayari kuanguka,
4 Mpango wao ni kumwangusha tu mtu mwenye cheo;
Huufurahia uongo.
Kwa kinywa chao hubariki;
Kwa moyo wao hulaani.
5 Nafsi yangu, umngoje Mungu peke yake kwa utulivu.
Maana tumaini langu hutoka kwake.
6 Yeye tu ndiye mwamba wangu na wokovu wangu,
Ngome yangu, sitatikisika.
7 Kwa Mungu wokovu wangu,
Na utukufu wangu;
Mwamba wa nguvu zangu,
Na kimbilio langu ni kwa Mungu.
8 Enyi watu, mtumainini sikuzote,
Ifunueni mioyo yenu mbele zake;
Mungu ndiye kimbilio letu.
9 Hakika binadamu ni ubatili,
Na wenye cheo ni uongo,
Katika mizani huinuka;
Wote pamoja ni hafifu kuliko ubatili.
10 Msiitumainie dhuluma,
Wala msijivune kwa unyang'anyi;
Mali izidipo msiiangalie sana moyoni.
11 Mara moja amenena Mungu;
Mara mbili nimeyasikia haya,
Ya kuwa nguvu zina Mungu,
12 Na fadhili ziko kwako, Ee Bwana;
Maana ndiwe umlipaye kila mtu
Kulingana na haki yake.