Ombi la kuokolewa kutoka kwa adui
Kwa mwimbishaji: kwa ala za muziki zenye nyuzi. Zaburi ya Daudi.
1 Ee Mungu wa haki yangu, uniitikie niitapo;
Uliniokoa nilipokuwa katika shida;
Unifadhili na kuisikia sala yangu.
2 Enyi wanadamu, hadi lini utukufu wangu utafedheheka?
Je! Mtapenda ubatili na kutafuta uongo hadi lini?
3 Bali jueni ya kuwa BWANA amejiteulia mtauwa;
BWANA husikia nimwitapo.
4 Muwe na hofu wala msitende dhambi,
Tafakarini vitandani mwenu na kutulia.
5 Toeni dhabihu za haki,
Na kumtumaini BWANA.
6 Wengi husema, Nani atakayetuonesha mema?
BWANA, utuinulie nuru ya uso wako.
7 Umenitia furaha moyoni mwangu,
Kupita yao wanapozidishiwa nafaka na divai.
8 Katika amani nitajilaza na kupata usingizi mara,
Maana Wewe, BWANA, peke yako,
Ndiwe unijaliaye kukaa salama.