1 Nitakushukuru kwa moyo wangu wote,
Mbele ya miungu nitakuimbia zaburi.
2 Nitasujudu nikilikabili hekalu lako takatifu,
Nitalishukuru jina lako,
Kwa ajili ya fadhili zako na uaminifu wako,
Kwa maana umeikuza ahadi yako,
na jina lako juu ya vyote.
3 Siku ile niliyokuita uliniitikia,
Ukanifariji nafsi kwa kunitia nguvu.
4 Ee BWANA, wafalme wote wa dunia watakushukuru,
Watakapoyasikia maneno ya kinywa chako.
5 Naam, wataziimba njia za BWANA,
Kwa maana utukufu wa BWANA ni mkuu.
6 Ingawa BWANA yuko juu, anamjali mnyenyekevu,
Naye amjua mwenye kujivuna tokea mbali.
7 Nijapopitia katika shida,
Unanilinda juu ya hasira ya adui zangu,
Unaunyosha mkono wako,
Na mkono wako wa kulia unaniokoa.
8 BWANA atanitimizia malengo yake kwangu;
Ee BWANA, fadhili zako ni za milele;
Usiiache kazi ya mikono yako.