1 Mpeni BWANA, enyi wana wa Mungu,
Mpeni BWANA utukufu na nguvu;
2 Mpeni BWANA utukufu wa jina lake;
Mwabuduni BWANA kwa uzuri wa utakatifu.
3 Sauti ya BWANA inasikika juu ya maji;
Mungu wa utukufu apiga radi;
BWANA yu juu ya maji mengi.
4 Sauti ya BWANA ina nguvu;
Sauti ya BWANA ina utukufu;
5 Sauti ya BWANA yaivunja mierezi;
Naam, BWANA aivunjavunja mierezi ya Lebanoni;
6 Airusharusha Lebanoni kama ndama wa ng'ombe;
Lebanoni na Sirioni kama mwananyati.
7 Sauti ya BWANA inatoa miale paa ya moto;
8 Sauti ya BWANA yalitetemesha jangwa;
BWANA alitetemesha jangwa la Kadeshi.
9 Sauti ya BWANA yawazalisha ayala,
Na kuiacha misitu wazi;
Na ndani ya hekalu lake
Wanasema, Utukufu!
10 BWANA aketi juu ya Gharika;
Naam, BWANA ameshika hatamu ya ufalme milele.
11 BWANA na awape watu wake nguvu;
BWANA na awabariki watu wake kwa amani.