1 Ee Mungu, uisikilize sala yangu,
Wala usijifiche nikuombapo rehema.
2 Unisikilize na kunijibu,
Nimetangatanga nikilalama na kuugua.
3 Kwa sababu ya sauti ya adui,
Kwa sababu ya dhuluma yake yule mwovu.
Kwa maana wananitupia uovu,
Na kwa ghadhabu wananiudhi.
4 Moyo wangu unaumia ndani yangu,
Na hofu za mauti zimeniangukia.
5 Hofu na tetemeko limenijia,
Na hofu kubwa imeniingia.
6 Nikasema, Ningekuwa na mbawa kama njiwa,
Ningeruka mbali na kustarehe.
7 Ningekwenda zangu mbali,
Ningetua jangwani.
8 Ningefanya haraka kuzikimbia
Dhoruba na tufani.
9 Ee Bwana, uwaangamize, uzivuruge ndimi zao,
Maana nimeona dhuluma na fitina katika mji.
10 Mchana na usiku huzunguka kutani mwake;
Uovu na taabu zimo ndani yake;
11 Tamaa mbaya zimo ndani yake;
Dhuluma na hila haziondoki mitaani mwake.
12 Kwa maana si adui aliyenitukana;
Kama ndivyo, ningevumilia.
Aliyejitukuza juu yangu siye anichukiaye;
Kama ndivyo, ningejificha asinione.
13 Bali ni wewe, mtu mwenzangu,
Rafiki yangu, niliyejuana nawe sana.
14 Tumehusiana vizuri; na kutembea
Nyumbani mwa Mungu pamoja na mkutano.
15 Mauti na iwapate kwa ghafla,
Na washuke kuzimu wangali hai,
Maana uovu uko nyumbani mwao moyoni mwao.
16 Nami nitamwita Mungu,
Na BWANA ataniokoa;
17 Jioni, asubuhi, na adhuhuri nitalalama na kuugua,
Naye ataisikia sauti yangu.
18 Ameiokoa nafsi yangu iwe salama, asinikaribie mtu,
Maana walioshindana nami walikuwa wengi.
19 Mungu atawalaye tangu milele atanisikia;
Na kuwaadhibu,
maana hawajirekebishi,
Wala kumcha Mungu.
20 Mwenzangu amenyosha mkono awadhuru waliopatana naye,
Amelivunja agano lake.
21 Kinywa chake ni laini kuliko siagi,
Bali moyo wake ni vita.
Maneno yake ni mororo kuliko mafuta,
Lakini yanakata kama upanga mkali.
22 Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza,
Hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.
23 Nawe, Ee Mungu, utawateremsha,
Wafikie shimo la uharibifu;
Watu wa damu na hila hawataishi nusu ya siku zao,
Bali mimi nitakutumaini Wewe.